KUSOMA KITABU CHA ZABURI {DAY 06}

| Makala

KUSOMA KITABU CHA ZABURI 

      DAY 06

Zaburi 26

1  Ee Bwana, unihukumu mimi, Maana nimekwenda kwa ukamilifu wangu, Nami nimemtumaini Bwana bila wasiwasi.

2  Ee Bwana, unijaribu na kunipima; Unisafishe mtima wangu na moyo wangu.

3  Maana fadhili zako zi mbele ya macho yangu, Nami nimekwenda katika kweli yako.

4  Sikuketi pamoja na watu wa ubatili, Wala sitaingia mnamo wanafiki.

5  Nimelichukia kusanyiko la watenda mabaya, Wala sitaketi pamoja na watu waovu.

6  Nitanawa mikono yangu kwa kutokuwa na hatia, Na kuizunguka madhabahu yako, Ee Bwana

7  Ili niitangaze sauti ya kushukuru, Na kuzisimulia kazi zako za ajabu.

8  Bwana, nimependa makao ya nyumba yako, Na mahali pa maskani ya utukufu wako.

9  Usiiondoe nafsi yangu pamoja na wakosaji, Wala uhai wangu pamoja na watu wa damu.

10  Mikononi mwao mna madhara, Na mkono wao wa kuume umejaa rushwa.

11  Ila mimi nitakwenda kwa ukamilifu wangu; Unikomboe, unifanyie fadhili.

12  Mguu wangu umesimama palipo sawa; Katika makusanyiko nitamhimidi Bwana.


 

Zaburi 27

1  Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani?

2  Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka.

3  Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.

4  Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake.

5  Mradi atanisitiri bandani mwake siku ya mabaya, Atanisitiri katika sitara ya hema yake, Na kuniinua juu ya mwamba.

6  Na sasa kichwa changu kitainuka Juu ya adui zangu wanaonizunguka. Nami nitatoa dhabihu za shangwe hemani mwake; Nitaimba, naam, nitamhimidi Bwana.

7  Ee Bwana, usikie, kwa sauti yangu ninalia, Unifadhili, unijibu.

8  Uliposema, Nitafuteni uso wangu, Moyo wangu umekuambia, Bwana, uso wako nitautafuta.

9  Usinifiche uso wako, Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira. Umekuwa msaada wangu, usinitupe, Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu.

10  Baba yangu na mama yangu wameniacha, Bali Bwana atanikaribisha kwake.

11  Ee Bwana, unifundishe njia yako, Na kuniongoza katika njia iliyonyoka; Kwa sababu yao wanaoniotea;

12  Usinitie katika nia ya watesi wangu; Maana mashahidi wa uongo wameniondokea, Nao watoao jeuri kama pumzi.

13  Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana Katika nchi ya walio hai.

14  Umngoje Bwana, uwe hodari, Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana.


 

Zaburi 28

1  Ee Bwana, nitakuita Wewe, mwamba wangu, Usiwe kwangu kama kiziwi. Nisije nikafanana nao washukao shimoni, Ikiwa umeninyamalia.

2  Uisikie sauti ya dua yangu nikuombapo, Nikipainulia patakatifu pako mikono yangu.

3  Usinikokote pamoja na wasio haki, Wala pamoja na watenda maovu. Wawaambiao jirani zao maneno ya amani, Lakini mioyoni mwao mna madhara.

4  Uwape sawasawa na vitendo vyao, Na kwa kadiri ya ubaya wa kufanya kwao, Uwape sawasawa na kazi ya mikono yao, Uwalipe stahili zao.

5  Maana hawazifahamu kazi za Bwana, Wala matendo ya mikono yake. Atawavunja wala hatawajenga;

6  Na ahimidiwe Bwana. Maana ameisikia sauti ya dua yangu;

7  Bwana ni nguvu zangu na ngao yangu. Moyo wangu umemtumaini, Nami nimesaidiwa; Basi, moyo wangu unashangilia, Na kwa wimbo wangu nitamshukuru.

8  Bwana ni nguvu za watu wake, Naye ni ngome ya wokovu kwa masihi

9  Uwaokoe watu wako, uubariki urithi wako, Uwachunge, uwachukue milele.



 

Zaburi 29

1  Mpeni Bwana, enyi wana wa Mungu, Mpeni Bwana utukufu na nguvu;

2  Mpeni Bwana utukufu wa jina lake; Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu.

3  Sauti ya Bwana i juu ya maji; Mungu wa utukufu alipiga radi; Bwana yu juu ya maji mengi.

4  Sauti ya Bwana ina nguvu; Sauti ya Bwana ina adhama;

5  Sauti ya Bwana yaivunja mierezi; Naam, Bwana aivunja-vunja mierezi ya Lebanoni;

6  Airusha-rusha kama ndama wa ng'ombe; Lebanoni na Sirioni kama mwana-nyati.

7  Sauti ya Bwana yaipasua miali ya moto;

8  Sauti ya Bwana yalitetemesha jangwa; Bwana alitetemesha jangwa la Kadeshi.

9  Sauti ya Bwana yawazalisha ayala, Na kuifichua misitu; Na ndani ya hekalu lake Wanasema wote, Utukufu.

10  Bwana aliketi juu ya Gharika; Naam, Bwana ameketi hali ya mfalme milele.

11  Bwana atawapa watu wake nguvu; Bwana atawabariki watu wake kwa amani.


 

Zaburi 30

1  Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua, Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu.

2  Ee Bwana, Mungu wangu, Nalikulilia ukaniponya.

3  Umeniinua nafsi yangu, Ee Bwana, kutoka kuzimu. Umenihuisha na kunitoa Miongoni mwao washukao shimoni.

4  Mwimbieni Bwana zaburi, Enyi watauwa wake. Na kufanya shukrani. Kwa kumbukumbu la utakatifu wake.

5  Maana ghadhabu zake ni za kitambo kidogo, Katika radhi yake mna uhai. Huenda kilio huja kukaa usiku, Lakini asubuhi huwa furaha.

6  Nami nilipofanikiwa nalisema, Sitaondoshwa milele.

7  Bwana, kwa radhi yako Wewe uliuimarisha mlima wangu. Uliuficha uso wako, Nami nikafadhaika.

8  Ee Bwana, nalikulilia Wewe, Naam, kwa Bwana naliomba dua.

9  Mna faida gani katika damu yangu Nishukapo shimoni? Mavumbi yatakusifu? Yataitangaza kweli yako?

10  Ee Bwana, usikie, unirehemu, Bwana, uwe msaidizi wangu.

11  Uligeuza matanga yangu kuwa machezo; Ulinivua gunia, ukanivika furaha.

12  Ili utukufu wangu ukusifu, Wala usinyamaze. Ee Bwana, Mungu wangu, Nitakushukuru milele.


 


 SADAKA